read

Aya 61: Si Vibaya Kwa Kipofu

Maana

Wanaombiwa katika neno 'Mliowashikia' ni walio na utawala kwenye mali kwa usimamizi, wasiya au wakala. Maana ya dhairi ya Aya ni kuwa hakuna ubaya kwa kipofu, kiguru, mgonjwa na wengineo kula bila ya kuomba ruhusa, kwenye majumba ya ndugu zao waliotajwa, wakiwa pamoja na wenye nyumba au peke yao. Vile vile si vibaya kwa wakili kula kwa wema mali aliyowakilishwa; kama ambavyo si vibaya kwa rafiki kula nyumbani kwa rafiki yake.
Wote hawa wanaweza kula katika majumba haya kwa sharti la kutojua kuwa wenyewe hawataki. Mafakihi wengi wanasema anayoruhusa ya kula matunda, saladi au chakula kilichokwishaandaliwa, lakini sio kile ambacho kimewekwa akiba.

Unaweza kuuliza kuwa neno 'Wala kwenu nyinyi mkila kwenye nyumba zenu' inafahamisha kuwa mtu anaweza kula nyumbani kwake bila ya kujiomba ruhusa yeye mwenyewe. Maneno hayaendi sawa hapa, itakuwaje?

Jibu: Makusudio yake ni nyumba ya mke na ya mtoto, kutokana na kauli yake Mwenyezi Mungu Mtukufu:

جَعَلَ لَكُمْ مِنْ أَنْفُسِكُمْ أَزْوَاجًا وَمِنَ الْأَنْعَامِ أَزْوَاجًا ۖ {11}

"Na amewajaalia mke na mume kutokana na nyinyi wenyewe." (42:11).

Kuna Hadith isemayo: "Chema zaidi anachokula mtu ni chumo lake." Na mtoto ni chumo lake, kutokana na Hadith nyingine isemayo: "Wewe na mali yako ni wa baba yako."

Swali la pili: Kwa nini Mwenyezi Mungu (s.w.t.) amehusisha kuwataja vipofu walemavu na wagonjwa, na wao wanaingia kwenye neno 'nyinyi wenyewe.' Kwa sababu wanambiwa watu wote. Sasa kwani kuna mtu atakayetia wasiwasi kwa walemavu hao waliotajwa na wagonjwa, kuwa hawafai kula kwenye hizo nyumba?

Kuna kauli nyingi za majibu ya swali hili. Wafasiri wengine wametaja tano. Iliyo karibu zaidi ni ile isemayo kuwa maswahaba walikuwa wakiona uzito kula na vipofu kwa kuwa hawatoweza kuona chakula kinachofaa, wasije wakala mapumba. Na kiguru waliona kuwa atapata tabu ya kukaa na wengine kwa vile chakula kilikuwa kinawekwa chini na mgonjwa naye hawezi kushiriki vizuri kula na wengine, ambapo wenzake watamaliza haraka naye ataona haya kubaki peke yake.

Kwa kuwa maswahaba walikuwa hawali katika majumba haya yaliyotajwa kutokana na Aya isemayo: "Wala msile mali zenu baina yenu kwa batili." Juz.1 (2:88). Ndipo Mwenyezi Mungu akawahalalishia kula kwenye majumba hayo, pamoja na kula na walemavu hao na wagonjwa.

إِنَّمَا الْمُؤْمِنُونَ الَّذِينَ آمَنُوا بِاللَّهِ وَرَسُولِهِ وَإِذَا كَانُوا مَعَهُ عَلَىٰ أَمْرٍ جَامِعٍ لَمْ يَذْهَبُوا حَتَّىٰ يَسْتَأْذِنُوهُ ۚ إِنَّ الَّذِينَ يَسْتَأْذِنُونَكَ أُولَٰئِكَ الَّذِينَ يُؤْمِنُونَ بِاللَّهِ وَرَسُولِهِ ۚ فَإِذَا اسْتَأْذَنُوكَ لِبَعْضِ شَأْنِهِمْ فَأْذَنْ لِمَنْ شِئْتَ مِنْهُمْ وَاسْتَغْفِرْ لَهُمُ اللَّهَ ۚ إِنَّ اللَّهَ غَفُورٌ رَحِيمٌ {62}

Hakika waumini ni wale tu ambao wamemwamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake na wakiwa pamoja naye kwa jambo la wote, hawaondoki mpaka wamtake ruhusa. Hakika wale wanaokuomba ruhusa, hao ndio wanaomwamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na watakapokuomba ruhusa kwa baadhi ya mambo yao, mruhusu umtakaye miongoni mwao na uwaombee msamaha kwa Mwenyezi Mungu; hakika Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa msamaha, Mwenye kurehemu.

لَا تَجْعَلُوا دُعَاءَ الرَّسُولِ بَيْنَكُمْ كَدُعَاءِ بَعْضِكُمْ بَعْضًا ۚ قَدْ يَعْلَمُ اللَّهُ الَّذِينَ يَتَسَلَّلُونَ مِنْكُمْ لِوَاذًا ۚ فَلْيَحْذَرِ الَّذِينَ يُخَالِفُونَ عَنْ أَمْرِهِ أَنْ تُصِيبَهُمْ فِتْنَةٌ أَوْ يُصِيبَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ {63}

Msifanye kumwita Mtume baina yenu kama mnavyoitana nyinyi kwa nyinyi. Hakika Mwenyezi Mungu anawajua miongoni mwenu wale wanoondoka kwa kujificha. Basi na watahadhari wale ambao wanahalifu amri yake, isije ikawapata fitna au ikawapata adhabu chungu.

أَلَا إِنَّ لِلَّهِ مَا فِي السَّمَاوَاتِ وَالْأَرْضِ ۖ قَدْ يَعْلَمُ مَا أَنْتُمْ عَلَيْهِ وَيَوْمَ يُرْجَعُونَ إِلَيْهِ فَيُنَبِّئُهُمْ بِمَا عَمِلُوا ۗ وَاللَّهُ بِكُلِّ شَيْءٍ عَلِيمٌ {64}

Ehee! Hakika ni vya Mwenyezi Mungu vilivyomo mbinguni na ardhini. Hakika yeye anajua mliyo nayo. Na siku watakaporudishwa kwake atawaeleza waliyoyafanya. Na Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa kila kitu.