Aya 94 – 96: Watawatolea Udhuru
Maana
Watawatolea udhuru mtakaporudi kwao.
Mfumo wa Aya unafahamisha kwamba Aya ilishuka wakati wa kurudi jeshi la Kiislamu kutoka vita ya Tabuk pale Mwenyezi Mungu alipowafahamisha kuwa watakapofika Madina, wanafiki watawakabili na nyudhuru kwa kukaa kwao nyuma. Watatoa nyudhuru za uwongo. Kwa hiyo Mwenyezi Mungu akamwambia Mtume wake:
Sema, msitoe udhuru; hatutawaamini. Mwenyezi Mungu amekwishatueleza habari zenu.
Huu ni ukatazo kutoka kwake Mwenyezi Mungu mtukufu kutokubali udhuru kutoka kwa wanafiki, na ni amri kwa Mtume (s.a.w.) awaambie kuwa sisadiki chochote katika mnayonitolea udhuru.
Kwa sababu Mwenyezi Mungu amenipa wahyi yale yanayofichwa na nyoyo zenu miongoni mwa shari na unafiki.
Na Mwenyezi Mungu na Mtume wake, ataviangalia vitendo vyenu.
Yaani hatukubali nyudhuru zenu mpaka mthibitishe kwa vitendo sio kwa maneno kwamba nyinyi ni wa kweli katika nia zenu na malengo yenu, na wenye ikhlasi katika kumwamini Mwenyezi Mungu kama mnavyodai.
Kisha mtarudishwa Mjuzi, wa ghaibu na dhahiri awaambie mliyokuwa mkiyatenda.
Ghaibu ni yale tusiyoyajua, yanajuliwa na Mwenyezi Mungu.
Maana ni kuwa nyinyi kesho mtasimama mbele ya Mwenyezi Mungu, ambaye halijifichi kwake la kujificha, awape habari ya matendo yenu na awalipe. Ikiwa ni heri basi ni heri na ikiwa ni shari basi ni shari.
Watawaapia Mwenyezi Mungu mtakaporudi kwao ili muachane nao.
Yaani mtakaporudi kutoka katika vita vya Tabuk. Ili muachane nao; yaani mnyamazie unafiki wao ni msiwatahayarize.
Basi achaneni nao.
Yaani wapuuzeni na muwadharau. Baadhi ya wapokezi wanasema kwamba Mtume (s.a.w.) aliwaamuru waislamu wasiwe na mawasiliano nao. Kisha Mwenyezi Mungu akabainisha sababu ya kuwapuuza na kuwadh rau kwa kauli yake:
Hakika wao ni uchafu, na makazi yao ni Jahanamu; ni malipo ya yale waliyokuwa wakiyachuma.
Kuna Hadith isemayo: “Tahadharini na kukaa na mauti.” Akaulizwa ni nani hao ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu. Akasema: Kila mwenye kupotewa na imani mjeuri wa hukumu.” Hadith nyingine inasema: “Mwenye hekima zaidi katika watu ni yule anayemkimbia mjinga zaidi katika watu.”
Wanawaapia ili muwe radhi nao. Kama mkiwa radhi nao, basi hakika Mwenyezi Mungu hatakuwa radhi na watu mafasiki.
Aina hii ya kukataza kwa upole ni mfumo fasaha zaidi. Kuwa radhi Waumini kunatokana na radhi ya Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu hawi radhi na watu mafasiki.
Sasa vipi Waumini wawe radhi nao? Yeyote anayedai kumwamini Mwenyezi Mungu huku akiwa radhi na yule aliyeghadhabikiwa na Mwenyezi Mungu basi yeye ni mnafiki, hilo halina shaka.
الْأَعْرَابُ أَشَدُّ كُفْرًا وَنِفَاقًا وَأَجْدَرُ أَلَّا يَعْلَمُوا حُدُودَ مَا أَنْزَلَ اللَّهُ عَلَىٰ رَسُولِهِ ۗ وَاللَّهُ عَلِيمٌ حَكِيمٌ {97}
وَمِنَ الْأَعْرَابِ مَنْ يَتَّخِذُ مَا يُنْفِقُ مَغْرَمًا وَيَتَرَبَّصُ بِكُمُ الدَّوَائِرَ ۚ عَلَيْهِمْ دَائِرَةُ السَّوْءِ ۗ وَاللَّهُ سَمِيعٌ عَلِيمٌ {98}
وَمِنَ الْأَعْرَابِ مَنْ يُؤْمِنُ بِاللَّهِ وَالْيَوْمِ الْآخِرِ وَيَتَّخِذُ مَا يُنْفِقُ قُرُبَاتٍ عِنْدَ اللَّهِ وَصَلَوَاتِ الرَّسُولِ ۚ أَلَا إِنَّهَا قُرْبَةٌ لَهُمْ ۚ سَيُدْخِلُهُمُ اللَّهُ فِي رَحْمَتِهِ ۗ إِنَّ اللَّهَ غَفُورٌ رَحِيمٌ {99}