read

Mwanamke Wa Dini; Majukumu Na Wajibu Wake

“...Mwenyezi Mungu amewaumba kutokana na nafsi moja...” (7:189)

Wajibu na majukumu ya mwanamke ni kama ya mwanamume, na suala lake ni kama la mume yaani suala la haki, ujumbe na marejeo. Isitoshe, mustakbali wa kazi yoyote ni dini kwa njia moja au nyengine mwanamke naye ana kazi yake.

Kuna kazi zingine ambazo hakuna awezaye kuzisimamia na kuzitekeleza ila yeye, kwa maana hiyo, huwezi kupata harakati zozote zenye kufaulu ila mwanamke atakuwa na fungu lake kubwa humo.

Ushahidi wa hayo ni mapinduzi ya Iran. Kuanzia hapa ndio pamekuwa na haja ya kuweka picha bora zaidi kwa mwanamke; vipi anapaswa awe, nini wajibu na majukumu yake, ndipo hapo tutajaribu kufafanua.

Majukumu Ya Mwanamke

“...Lau si waumini wanaume na waumini wanawake...” (48:25)

Kazi inayompasa kufanya mwanamke wa kidini siyo zawadi anayopewa na mwanamume (akikataa kumpa, basi) bali ni miongoni mwa haki zake na ni miongoni mwa majukumu yake kwa hiyo ni juu yake atekeleze majukumu yake. Vinginevyo, hatakubaliwa atoe udhuru mbele ya Mwenyezi Mungu na Historia kwamba wanaume hawakumwachia atimize wajibu wake wala hawakumpa kazi ya kufanya kwenye utekelezaji huo.

Kwa hivyo ni lazima mwanamke huyo ajihisabu kuwa yumo kwenye kutekeleza wajibu wake kwa kujitolea nafsi yake kwenye upande wa mapambano kwa kuinua kiwango chake cha kifikra, kisiasa, kielimu, kidini na kikazi.

Inapasa achukue mfano wa wapiganaji jihadi wakubwa wa kike kama Bibi Khadija Al- Kubra, Bibi Fatima Zahra, Bibi Zainab Al-Kubra na wengineo.

Inapasa mwanamke atangulie na awe mbele ya mwanamume katika kubeba majukumu na wakati huo huo katika kuusimamisha Uislamu. Kwa sababu mwanamke hutangulia hata katika kubaleghe ‘kisharia’ kabla ya mwanamume kwa miaka minne; vilevile katika kufanya kazi na kutekeleza wajibu atangulie.

Kama twajua kwamba miongoni mwa matawi ya dini ni kuamrisha mema na kukataza maovu, kuwapenda wanaopenda kizazi cha Mtume (saww) na kuwachukia maadui wa kizazi hicho, na jihadi, na kwamba hayo yote ni wajibu kwa mwanamke na mwanamume. Basi, ni lazima tujue kwamba mwanamke ana kazi kubwa katika kufanya amali na jihadi kushinda mwanamume.

Katika Historia ni dhahiri kwamba mwanamke alifanya kazi kubwa katika zile siku ambazo Uislamu ulipambana kujenga maisha mapya. Lakini, hizi siku zote za sasa za kutoendelea zimefanya mwanamke awe mbali na mapambano na zimempokonya majukumu yake ya kimapinduzi mpaka kufikia mwanamke kuwa ni mateka, mpishi tu au yaya wa kulea watoto.

Na kwa kila mwanadamu anapendelea awe ametekeleza wajibu fulani katika maisha na nafsi yake inamsukuma kufanya hivyo. Lakini, mwanamke wetu hajapata nafasi yake ila tu katika nafasi za wacheza sinema au waimbaji na wale wanawake wetu wema wamekaa majumbani wakingojea mtu wa kumpa zawadi ya “kazi ya kufanya”; asipokuja wa kufanya hivyo basi huachwa nje.

Lazima mwanamke, ili kurekebisha hali hii, afanye kazi maradufu. Tunaamini kwamba anaweza. Suala hapa la kujiuliza ni, Je! vielelezo vyenyewe ni vipi?

Mwanamke Katika Ujumbe Wa Mwenyezi Mungu

“Na waumini wanaume na waumini wanawake ni marafiki wao kwa wao..” (9:71)

Mwanamke mu’umin, katika ujumbe wa Mungu, siyo yule kiumbe dhaifu mwoga, mwenye kujitenga na uwanja wa mapambano, bali ni yule mwanamke aliyejitokeza mbele, jasiri, mwenye vitendo, mwenye kutengeza mustakbali wake na wa vizazi vijavyo, mwenye ukakamavu la muda mrefu kwenye njia ya haki, uadilifu, uhuru na kuinua neno la Mungu.

Mwanamke anapokuwa katika ujumbe wa Mungu yeye ni mume, hapana tofauti kwani yeye amekuwa bega kwa bega na Manabii katika mapambano kama tutakavyoona katika Qur’an. Mwenyezi Mungu anawapigia kuwa ni ‘mifano’ na ‘walioamini’ tutataja hapa baadhi ya mifano:

Adam Na Hawa

Mtu na Mtume wa kwanza kabisa, Adam, tunaona kando yake kuna Mwanamke, Hawa.

Hawa huyu alikuwa na safari ya taabu na ndefu na mumewe Adam na Ibilisi, tangu peponi hadi kuteremshwa duniani.

Katika kuumbwa walikuwa pamoja, Mwenyezi Mungu akamuumba …“Na akamuumbia mkewe kutokana na nafsi ile ile…” ( 4:1)

Walikuwa pamoja walipokutana na Ibilisi. Walibeba majukumu pamoja na wamepokea mwongozo pamoja.
Mwenyezi Mungu anasema katika Qur’an “Na tulisema: “Ewe Adam! Kaa wewe na mkeo katika bustani hii (peponi), na kuleni humo maridhawa popote mpendapo, lakini msiukaribie mti huu tu; msije kuwa miongoni mwa waliodhulumu (nafsi zao). Shetani aliwatelezesha wote wawili, na akawatoa katika ile (hali) waliyokuwa nayo. Tukawaambia “Nendeni hali ya kuwa maadui nyinyi kwa nyinyi, na makazi yenu (sasa) katika ardhi, na (mtapata) starehe humo kwa muda (mahsusi) (2: 35–36)

“Tukasema: Shukeni humo nyote; na kama ukikufikieni uongozi utokao kwangu, basi watakaofuata uongozi wangu huo haitakuwa khofu juu yao wala hawata­huzunika.” (2:38)

Kwa hivyo msafara wa Adam na Hawa ulikuwa mmoja, na kubeba majukumu kulikuwa kumoja na matokeo pia yalikuwa mamoja. Aidha, mapambano kati ya Ibilisi na ‘mtu’ awe mume au mke – ni mmoja.

“…Tukasema, Ewe Adam! Huyu (Ibilisi) ni adui kwako na kwa mkeo.” (20:117)

Hivi ndivyo Mwanamke aliyokuwapo kwa kujitokeza tangu mwanzo wa kuumbwa.

Mwanamke Hajar na Ibrahim (a.s)

Huyu ni Mwanamke jasiri, mwenye nia safi aliyeihama nyumba yake na nchi yake ili aende akaishi kando ya nyumba ya Mungu katika ardhi kame isiyo na maji wala manyasi ili amwabudu Mungu pekee na ajitenge na kuabudu watu. Nabii Ibrahim alisema:

Mola wetu! Hakika mimi nimewaweka (Ismail na mamaye) katika bonde (hili, Makka) lisilokuwa na mimea yoyote, katika nyumba yake takatifu (Al-Kaaba) Mola wetu! Wajaalie wasimamishe Swala. Na ujaalie nyoyo za watu zielekee kwao na uwaruzuku ili wapate kushukuru.” (14:37)

Bibi huyu Hajar alisumbuka na kwenda mbio kwa ajili ya kumtafutia maji mwanawe akienda mbio kati ya Swafa na Marwa; kukimbia huko kukawa ni kielelezo cha kufanya kazi kwa ajili ya kuwatafutia maisha wengine. Naye alimlea Ismail (a.s) malezi ya kidini yaliyomfanya anyenyekee na kukubali kukipokea kifo kwa mikono miwili pale alipoambiwa na babake.

“Mimi nimeota usingizini kuwa nakuchinja.” Jibu la Ismail lilikuwa: “Ewe baba! Fanya uliloamrishwa (na Mwenyezi Mungu) utanipata mimi Inshallah ni miongoni mwa wanaosubiri.” (37:102)

Musa pamoja na Asya

Miongoni mwa picha njema za mwanamke katika ujumbe wa Mungu ni picha ya Bi Asya bint Muzahim, mke wa Dikteta Firaun.

Mwanamke huyu mcha Mungu alikuwa ndiye ngome kuu ya Nabii Musa bin Imran (a.s) tangu alipozaliwa; pale alipotiwa majini na mamake, akaokotwa na wafanya kazi wa Firaun naye akataka kumuuwa, Asya akamzuia; kama Qur’an inayotuelezea:

“Basi wakamwokota watu wa Firaun, ili awe adui kwao na huzuni; bila shaka Firaun na Hamana na majeshi yao walikuwa wenye uovu.” (28:8)

Iliwezekana Firaun amuuwe Musa mara moja lakini kuingilia kati kwa mkewe (Asya) ndiko kuliko­muokoa Musa na kifo.

“Na mkewe Firaun alisema’ (Usimuuwe) atakuwa kibu­rudisho cha macho kwangu na kwako, na msimuuwe, huenda atatunufaisha au tumpange kuwa mtoto (wetu).” (28:9)

Msimamo huo wa Bi Asya haukuwa kwa Musa tu, bali alikuwa - kama mapokezi yasemavyo – ni mama wa Waislamu wote, akiwahurumia, akiwatetea na kuwakirimu kwa sadaka.

Ndio, alikuwa mke wa Firaun, lakini mapenzi yake yalikuwa ni kupenda haki na ibada zake ni kumwabudu Mungu pekee, na ujasiri wake ni kupigania dini, kwa hivyo alikuwa ni adui wa taghuti Firaun kutokea ndani.

Utukufu ulioje aliokuwa nao wa kuweza kutohadaika na anasa alizokuwa nazo mumewe na kushikamana na Mtume aliye adui wa mumewe? Milki, na utajiri wa mito ipitayo kwenye ardhi ya nchi ya Misri ndivyo vilivyoiteka akili ya Firaun mtawala wa ki-imla hata akajifanya Mungu, akatangaza wazi wazi kuwa ‘Mimi ndiye Mungu wenu Mkuu”, lakini muangalie huyu mwanamke aliyekuwa akiishi naye na kulala naye kitanda kimoja na kuneemeka na neema alizo nazo mumewe na heshima anazopatiwa (za kuwa mke wa Firaun); pamoja na hayo yote yeye alikuwa muúmin na mchaji, hata akaweza kusimama pamoja na haki na kukataa udikteta.

Aliyakataa maisha ya Firaun kwa sababu yalikuwa ni ya dhulma na ujuba, licha ya kuwa yeye ndiye angelikuwa wa kwanza kufaidika nayo! …Hebu mwangalie akiinua macho yake mbinguni akisema: “Ewe Mola! Nijengee nyumba peponi.”

Imepokewa kwenye Hadith kwamba kisha: “Firaun alimfunga mikono yake na miguu yake kwa vigingi vinne, akamlaza juani, kisha akaamrisha atupwe jabalini, hatimaye akafa.” Kwa hivyo alikufa shahid.

Kwa hatima yake hii, Asya amekuwa ni kielelezo cha mwanamke wa kidini, na kielelezo cha wote wanaofuata njia ya haki, uadilifu na uhuru.

Mwenyezi Mungu anatupigia mfano:

“Na Mwenyezi Mungu amepiga mfano wa wale walioamini kweli, ni mkewe Firaun, aliposema: “Ee Mola wangu! Nijengee nyumba peponi na uniokoe na Firaun na amali zake na uniokoe na watu madhalimu.” (66:11)

Bi Maryam, Mama Yake Masih, Isa (a.s)

Bi Maryam: mwanamke mtukufu aliye juu ya maisha haya ya dunia na anasa zake.

Bi Maryam, aliyekataa njia ya Waisraili, mtetezi wa mihrabu ya ibada …aliyejitenga na jamii ya kimaada yenye misingi ya kuabudu pato na chumo la pesa.

Bibi huyu ndiye aliyejitolea kuyalinda maadili ya dini.

Maryam ni kielelezo kingine cha mwanamke mwanadini, kisa chake ni kipi? Jihadi yake ni ipi? Hebu tuangalie.”

Mamake Maryam alipojihisi kuwa mja mzito alimwambia Mungu:

“…Mola wangu! Nimeweka nadhiri kwako aliyomo tumboni mwangu kuwa wakfu, basi nikubalie. Bila shaka wewe ndiye usikiaye na ujuaye.” (3:35)

“Basi Mola wake akampokea (yule mtoto) kwa kabuli njema na akamkuza makuzi mema na akamfanya Zakariya awe mlezi wake.” (3:37)

Maryam alipokuwa, alishikamana na nadhiri ya mamake akaishi maisha ya utawa na ya kimapinduzi.

Alisimama imara na mwanawe mtukufu Isa (a.s) na akavumilia kila aina ya mateso, maudhi na tuhuma. Mwenyezi Mungu anasema:

“Na mtaje Maryam kitabuni (humo). Alipojitenga na jamaa zake, (akaenda) mahali upande wa Mashariki (wa msikiti). Na akaweka pazia kujikinga nao. Tukampeleka muhuisha sharia wetu (Jibril) akajimithilisha kwake (kwa sura ya) binadamu aliye kamili. Akasema (Maryam): Hakika mimi najikinga kwa Mwenyezi Mungu aniepushe nawe, ikiwa unamuogopa Mwenyezi Mungu. (Malaika) Akasema: “Hakika mimi ni mjumbe wa Mola wako ili nikupe mwana mtakatifu.
Akasema (Maryam) “nawezaje kupata mtoto hali sijaguswa na mwanamume (yeyote) na wala mimi si mzinifu?” Akasema (Malaika ) “Ni kama hivyo (usemavyo) Mola wako amesema haya ni sahali kwangu. Na ili tumfanye muujiza kwa watu na rehma itokayo kwetu. Na hili ni jambo lililokwisha hukumiwa.”
(19: 16-21)

Mwenyezi Mungu anaendelea kueleza kisa hiki; baada ya Isa (a.s) kuzaliwa:

“Akenda kwa jamaa zake amembeba. Wakasema: Ewe Maryam! Hakika umeleta jambo la ajabu! (kuzaa hivi hivi tu), ewe dada yake Harun! Baba yako hakuwa mtu mbaya wala mama yako hakuwa hasharati. (Maryam) akawaashiria kwake (yule mtoto). Wakasema: “Tuzun­gumze na aliye bado mtoto kitandani? (Yule mtoto) akasema: “Hakika mimi ni mja kwa Mwenyezi Mungu, amenipa kitabu na amenifanya Nabii. Na amenifanya mbarikiwa popote nilipo. Na ameniusia Swala na Zaka maadamu ni hai. Na ameniusia kufanya mema mama yangu, wala hakunifanya niwe jeuri, mwovu.” (19:27-32)

Basi hivi ndivyo alivyokuwa Maryam, nguzo ya Nabii Isa nanga ya mapinduzi yake. Alisimama naye bega kwa bega mpaka dakika ya mwisho ya maisha yake; mpaka wawili hawa wamechukuliwa na Mwenyezi Mungu kuwa ni muujiza mkubwa pale aliposema:

“Na tulilofanya mwana wa Maryam na mamake kuwa ishara na tukawapa makimbilio mahali palipoinuka…” (23:50)

Kwa nini? Kwa sababu Maryam alikataa kumnye­nyekea asiyekuwa Mungu akiwa katika mazingira magumu kwa ajili ya kuitikia mwito wa Mwenyezi Mungu kwake.

“Ewe Maryam! Mnyenyekee Mola wako na usujudu na urukuu pamoja na wanaorukuu.” (3:41)

Na hapa ndipo aliposifiwa, “Na Maryam mtoto wa Imran aliyejihifadhi nafsi (tupu) yake na tukampulizia humo roho yetu (inayotokana na sisi) na akayasadikisha maneno ya Mola wake, na vitabu vyake, na alikuwa miongoni mwa wanyenyekevu.” (66:12)

Bi Khadija na Mtume (saww)

Bi Khadija alikuwa akiamini ujumbe wa Mtume (saww) na wa kumtetea. Mtume (saww) alimuoa wakati bibi huyo akiwa na mali chungu nzima, alikuwa ni mmoja kati ya mamilionea wa Kiarabu. Mtume (saww) alipoteremshiwa wahyi, bibi huyu alitoa mali zake zote katika njia ya Mwenyezi Mungu mpaka ilifikia kufa kwa njaa na kiu katika wangwa wa pango la Abu Talib.

Hivi ndivyo alivyokuwa Khadija, mwanamapi­nduzi wa kwanza katika jamii kafiri ya Makka na ndiye wa kwanza katika kabila la Maqureish kuswali nyuma ya Mtume pamoja na Ali bin Abi Talib (a.s).

Hiyo ndiyo ilikuwa Swala ya kwanza kuswali katika Uislamu. Ilikuwa ni Swala ya kimapinduzi.

Na ilikuwa Swala ya kweli ya ‘Lailaha illa llah.’

Bibi huyu alishikamana na Swala hiyo mpaka hatima ya maisha yake katika miaka kumi ya mwanzo ambayo Mtume alikuwa akieneza ujumbe, alistahmili matatizo mazito kuwahi kutokea katika historia ya Kiislamu.

Mtume naye, baada ya kufa Bi Khadija, hakuwacha kutaja wasifu wake kwa jinsi alivyojitolea, ushujaa wake na misimamo yake, hata siku moja Aisha akaona wivu akasema: “..lakini Mweneyzi Mungu amekupa bora zaidi yake (huyo Khadija) “Hapo picha ya ushujaa wa Bi Khadija ikamjia Mtume machoni kwake akamkemea Aisha: “We! Usiseme hivyo! Mwenyezi Mungu hajanibadilishia aliye bora kuliko yeye, kwani alinisadiki wakati watu walinikadhibisha; akanisapoti katika dini ya Mwenyezi Mungu na akanisaidia kwa mali zake, na Mweneyzi Mungu ameniamrisha nimbashirie Khadija nyumba huko peponi.”

Ali (a.s) na Bi Fatima (a.s)

Fatima ndiye aliyeleta mapinduzi ndani ya mapinduzi pale wengine walipojaribu kuyabadilisha mapinduzi yawe dola. Yeye alikuwa kiongozi wa mapinduzi ya mageuzi, mbele ya nyuso za matapeli wa kisiasa walioyaiba mapinduzi ili wayafanyie biashara.

Yeye alikataa, akabisha, akakatilia mbali utawala, akajadiliana na khalifa na akaweza kumshinda kwa nguvu za hoja. Alipambana na kila aina ya mateso kwa ajili ya haki kama vile, kupigwa, kuharibika uja uzito wake na hata kuteketezwa nyumba yake. Na hakuishi katika kupinga tu, bali mlango wake ulikuwa wazi kwa wanamapinduzi, ndipo akawa ni mwanamke wa kwanza katika uislamu kupinga wizi wa nembo za kiislamu. Huyo ndiye Fatima (a.s).

Husein (a.s) pamoja na Zainab (a.s)

Bi Zainab alikuwa mwenziwe Husein katika mapi­nduzi na mtetezi wake katika kupigana Jihad, vile­vile alikuwa ni tegemeo lake na sauti yake kwa ma­milioni ya watu baada yake.

Ikiwa kila mapinduzi yana umwagikaji wa damu na ujumbe, basi damu iliyomwagika ni ya Husein, na ujumbe ni ule aliokuwa nao Zainab.

Sasa tufanye nini?

Jibu, ni kuchukuwa hatua zifuatazo!

Kuwe na maandalizi ya kutosha.

Yapasa mwanamke mwanadini ajiandae vya kutosha kutumia uwezo wake kwa kuwa Mwenyezi Mungu amempa kila mtu uwezo na vipaji vyake, lakini hivi kuna haja ya kuvigundua, kama Mwenyezi Mungu alivyoweka madini yenye thamani chini ya ardhi, lakini huwezi kufaidika nayo mpaka uyachimbe.

Ni kosa kubwa sana kwa watu au mtu kudharau kipaji na uwezo wake kwani Mwenyezi Mungu atatuuliza siku ya kiyama, kama alivyosema Mtume (saww): “Hatapita yeyote kwenye sirat miongoni mwenu, mpaka aulizwe kwanza jinsi alivyoupitisha umri wake na alivyomaliza ujana wake.”

Kwa hivyo kwa mwanamke yampasa kwanza kukuza uwezo na kipaji chake na leo ni kukuza uwezo wake binafsi wa uongozi, na hivyo ni kuweza kuwa na sifa zinazostahiki, mathalan; ushujaa, imani, subira na uongofu nt maadili ya kimapinduzi na harakati.

Atakapokuwa na sifa hizi pia itampasa akuze uwezo na kipaji chake katika uongozi, usemaji utunzi, mbinu za ushujaa na ajifunze kuendesha gari na pikipiki.

Uhusiano Wa Kadiri Na Mume

“Ziokoeni nafsi zenu na watu wenu kutokana na moto…” (66:6)

Mwanamke anapoingia kwenye maisha ya ndoa bado anakuwa na athari za maisha yake ya nyuma kabla hajaolewa ama kisaikolojia ama kitabia, kwa hivyo hapa itambidi abadilishe maisha yake, fikra zake na mazowea yake kulingana na mahitaji ya jambo analofanya na mumewe, na kwa tabia ya mwanamke iliyo, hawezi kuathirika haraka, kwa hivyo itampasa aanze safari ya kujibadilisha yeye mwenyewe kwanza kwa subira na upole.

Mwanamke asikate tamaa kwa uzito atakaopata wa­kati atakapokuwa akijirekebisha ili aende sambamba na maisha yake mapya.

Hapa kuna baadhi ya mambo muhimu ambayo yatamfaa mume na mke wakati wa maisha yao ya ndoa.

Lazima pawe na lugha moja katika masuala mbali mbali na hivyo kuwe na majadiliano ya kifikra, kisiasa na kidini baina yao. Na ikitokea mume akawa amemshinda mkewe katika mojawapo ya mambo haya, basi itambidi mke afanye bidii sana ili afikie kiwango cha mumewe, na vilevile mke akijiona anamshinda mumewe basi na amsaidie bila ya kujidai ili mume afikie kiwango chake.

Ni lazima mke ajue kuwa uhusiano wa kitandani tu hautoshi, kuimarisha uhusiano wao bali yapasa kuwe na uhusiano wa kimapambano.

Mwanamke mwanadini ajigeuze polepole kuwa sekretari wa kidini wa mumewe, amuandalie mazingira ya kumshujaisha mumewe atekeleze vizuri kazi na wajibu wake kama na kujisomea, kufanya kazi za huduma kwa jamii na nyinginezo, ampangie vizuri ofisi yake vile ipasavyo na akimkumbusha miadi yake na mtu, na mengineyo, lakini wakati huo huo asipekue na kuangalia vitu ambavyo mumewe hataki avione, kwani kuvumbua siri za mumewe ni haramu kisheria na lazima kutaleta madhara kwenye uhusiano wao.

Kuna msemo maarufu usemao “Nyuma ya kila mtu mashuhuri kuna mwanamke” kwa hivyo yapasa mwanamke mwanadini awe nyuma ya mumewe mwanadini ili awe mashuhuri mbele ya Mwenyezi Mungu na historia.

Kuwe na kusaidiana baina ya mume na mke katika mambo yote yawe ni ya kidini, ya kinyumbani au ya kibinafsi, kiasi kwamba kuwe na raghba ya kila mmoja kumsaidia mwenzake.

Mke apunguziwe mizigo ya kazi za nyumbani ili aweze kubeba vizuri kazi za kidini.

Washirikishwe katika kazi za dini kama vile kutengeneza mafaili yanayohusu mambo maalum.

Wafanye kikao rasmi juu ya kazi za dini na kila mtu maazimio yake yaheshimiwe.

“Ewe Mola! Tupe katika wake zetu na watoto wetu viburudisho vya macho yetu na utujaalie tuwe viongozi wa wacha mungu.” (25:74)

Wajibu Wa Kila Mmoja (Binafsi)

Kila mwanamke mwanadini inapasa pamoja na majukumu yake ya kijamii awe na majukumu yake binafsi akiyatekeleza kipekee nyumbani au mahali pengine.

Majukumu hayo ni kama ifuatayo:

Upande wa uandishi, mathalan, utungaji, uandishi wa makala na barua kwenye magazeti au vilevile kukusanya habari za magazeti kwa kifupi na kuandika kanda zilizorekodiwa (khutba n.k).

Kupiga chapa ya tapureta

Kutayarisha mafaili ya kuhifadhia matukio muhimu yale atakayoyaona kuwa yana faida

Kujisomea kila siku

Wajibu wa pamoja

“Sema : “ Fanyeni (kwa pamoja) ” (9:105)

Kabla hatujazungumza chochote kwenye suala hili, ni lazima kwanza tusisitize kwamba kufanya kazi kwa pamoja ni jambo linalohitajika sana katika mkondo huu wa historia ya umma wetu, kwa sababu umoja huzidisha nguvu kutokana na uwingi na kwamba Mungu yu pamoja na wengi.

Mtume alikuwa akisema mara kwa mara! “Wawili ni bora kuliko mmoja, na watatu ni bora kuliko wawili, na wanne ni bora kuliko watatu.”

Hapa, hata hivyo, kuna swali; hebu tufaradhie kuwa kuna wasichana wanadini ambao wapo tayari kushirikiana, lakini je! majukumu gani watakayoweza kuyatekeleza?

Jibu ni kwamba, majukumu watakayohitajika ku­yatekeleza ni haya:

Kuunda jumuia za kusimamia mambo ya dini, utafutaji pesa, muongozo na kuihamasisha jamii.

Kuunda jumuiya za kujitolea kwenye mambo ya kheri, kukusanya michango, kutoa misada na mengineyo.

Kuendesha mambo ya kielimu au ya kijamii k.v. kusimamia msikiti, kumbi za mikutano, maktaba, n.k. vilevile kutoa jarida maalum kwa mwanamke hata kama kwa kuanzia watoe vijinakala tu.

Kuandaa safari zenye manufaa.

Kushiriki kwenye harakati zote kwa ujumla, maandamano ya kidini n.k.

Haya ndiyo yapasayo kufanywa nao kwa ushirikiano katika kutekeleza wajibu wa pamoja.

Na ni vizuri tueleze hapa ya kwamba kushirikiana pamoja kati ya mwanamume na mwanamke na huku wakichunga sheria – sio kuwa inafaa tu bali pia ni muhimu sana.