Husaini Mwana wa Ali
Naanziliza kwa jina
Lake yeye Subhana
Mola asiye kijana
Wala mke asiliye
Ndie watangu natangu
Kabula ya ulimwengu
Muumba nchi na mbingu
Milele Atabakiya
Asie na mshirika
Na wala hakuzalika
Ameketi pasi shaka
Enzie imetimiya
Sasa penda kuweleza
Kisa chenye kuchukiza
Na moyo nitaukaza
Hadi mwisho kufikiya
Ni rafiki wa Rasuli
Muhammadi mur sali
Husaini mwana wa Ali
Na Fatima Hashimiya
Kipenzi chake Nabiya
Kuliko viumbe piya
Uhai wake sikia
Husaini akimwambiya
Wewe mtu wa peponi
Huna shaka asilani
Apendae kubaini
Namtizame Husaini
Baada kufa Rasuli
Muda ulipotawili
Na Alii mjamali
Alipoaga duniya
Kukazidi wasiwasi
Ulimwengu ukahisi
Pasiwe mwenye nafasi
Matumbo kupiganiya
Baada yote kufika
Na damu zikimwaika
Waso haya wakatoka
Vita wakaandaliya
Vikaandaliwa vita
Na mengi mno matata
Umbea nausalata
Vigaro vikatimiya
Vigaro vya mahasidi
Nyoyo zenye ufisadi
Chini ya yeye Yazidi
Vitani wakaingia
Husaini yuko ndiani
Kutaka ihami dini
Kuwapinga mashetani
Nakuituza duniya
Kwa moyo uso imani
Majeshi yakawa kani
Na damu waitamani
Ya Husaini na dhuriya
Wakawa wajikatakata
Watakayo washapata
Na Imamu washamwita
Mjini kwao kwingiya
Habari hiyo hanayo
Amekaza wake moyo
Kumbe mambo sasa siyo
Mauti yamngojea
Yunjiani enda zake
Akaweta watu wake
Waume na wanawake
Na radhi akawiliya
Kuwajuza kwa yakini
Hila zote kwa makini
Pasipo matumaini
Iraqi kufikiliya
Kawambiya kimbieni
Atakae samahani
Ila mimi niwacheni
Nimuhali kukimbiya
Baada yeye kukuli
Wengi hawakuhimili
Kama vile mafahali
Nyumbani wakarudia
Akabakiya Husaini
Na dhuriya wa nyumbani
Na baadhi ikhiwani
Akali wakasaliya
Alipofika Iraqi
Jamii ya halaiki
Furaha na kujinaki
Jeshi likamwingilia
Akawa hana namna
Pande zote amebanwa
Pamwe na wake vijana
Wapi watakimbiliya
Akasema kwa lafudhi
Kwa fasaha na mahadhi
Adui kuwapa radhi
Kuwatajia Jalia
Akawaonya mifano
Hati zao za mkono
Barua zilizo nono
Walizo kumwandikia
Kayesha yote maneno
Wala pasipo usono
Yote yasiwe ni neno
Yao wakashikilia
Wakamuonya adhabu
Na nyingi mno sulubu
Zimewaingia ghadhabu
Bila sababu ya njia
Adui pasi kuchoka
Wakamwandama M-maka
Karbala wakafika
Kusudi wa mwandamiya
Furati wakaushika
Pasi nafasi kutoka
Mto wakauzunguka
Na maji wakijinyweya
Kiu ikazidi sana
Na joto likawabana
Imamu na wake wana
Dhiki ikawadhidiya
Ikawa hakuna budi
Dhiki imeshawazidi
Wazee kwa auladi
Roho zikiteketea
Kiu ilo kubwa mno
Joto lisilo kifani
Vijana wazi midomo
Maji wanahitajiya
Maji wanywayo wanyama
Punda farasi na kima
Mjukuu wa Hashima
Adui akazuwiya
Akenda kwao salama
Karibu roho kutema
Abdallah anawana
Kwa kiu kumzidiya
Kile kijana swaghiri
Imamu wetu Amiri
Tamaa hakukasiri
Ya mali kumpatiya
Adui wasikubali
Japo lau tone mbili
Mahali wakaratili
Pasi imani kuingiya
Ndipo akikariri
Imamu akihubiri
Alipata takisiri
Chembe wakamrushiya
Wakamba ha ndiyo maji
Katu huyaonji maji
Mnyweshe yamfereji
Ni leo mtatubiya
Kijana kikalalama
Chembe limeshika nyama
Na damu mwili nzima
Mikononi kikafiya
Mikononi mwa Imamu
Yote ikajaa damu
Na roho yake ghulamu
Ikaiaga duniya
Katu wakamba adui
Maji yetu situmai
Mtayaona jamii
Kinywani hamtotiya
Ukazidi ukaidi
Kwa jeshi la mafisadi
Ikawa hapana budi
Roho zikiteketeya
Basi huu ndiyo mwanzo
Wakazidisha mikazo
Pasiwe hata pumbazo
Vitoto vikiumiya
Kajaribu kwa upole
Kuwaeleza walo pale
Maji yote yako tele
Japo tone kutumiya
Akenda huko karibu
Kiu ilimughilibu
Alipotaka jaribu
Chembe kikamuingiya
Kikamwingia Imamu
Chembe chao mahasimu
Mdomoni kikadumu
Na damu ikamweneya
Huku kiu imemshika
Damu ikichirizika
Msiba umemfika
Hana pakukimbiliya
Kakishika kakizuwa
Kwa nguvu akakitowa
Kamshukuru Molawa
Muumba wa waja piya
Zikazidishwa sulubu
Mno na nyingi taabu
Rafikize wakaghibu
Mauti kuyandamiya
Rafiki wakaanguka
Imamu kumzunguka
Na damu zikimwaika
Akawa aogeleya
Katikati kwenye damu
Adui wakakalimu
Katu yako hayatimu
Mauti yakungojeya
Mauti yenye taabu
Usumbufu na adhabu
Yatakufika karibu
Kaa ukiliadhaniya
Ni leo, leo ni leo
Utaiona kwa leo
Na wote hao watu
Wote tutawalemeya
Kakalimu muungwana
Kamshukuru Rabana
Na Molawe kalingana
Na dua kujiombeya
Akatamka Husaini
Kamwambia Mola manani
Kwako wewe shukrani
Nyoyo zimefurahiya
Hatuna katu huzuni
Kwa ulio yasaini
Mauti twayatamani
Kuliko kuangukiya
Vita vikauma sana
Pasipo kusemeyana
Na Imamu akawana
Pasi nyuma kurejeya
Lakini ifae nini
Kwa adui elfeni
Na ziyada ilondani
Husaini akalegeya
Akalegeya kwa dhiki
Aloikuta hilaki
Asimpate rafiki
Huruma kumuoneya
Ukweli ulodhihiri
Ikakabili ni shari
Haikuweko ni siri
Shida zikawachachiya
Kutamka kwa upole
Pasipo nyingi kelele
Sahibuze kuwambile
Atakaye kukiribiya
Usiku huo gizani
Kawambia kimbiyeni
Na mimi radhi moyoni
Na dua nawaombeya
Jamii wakakataa
Heri kwao kujifia
Kuliko kuyakimbia
Mauti wakaridhiya
Adui likadhihiri
Moyo umetahayari
Na upesi ikaswiri
Imamu kumjiliya
Mtoto wake Husaini
Naye alipobaini
Karuka pasi makini
Amie kumteteya
Pasi khofu wala shaka
Adui akamshika
Na maneno katamka
Msihaya kamwambiya
Kamwambiya huna haya
Bure wayatenda haya
Utaikuta hizaya
Mbele ya Mola jaliya
Adui likazunguka
Mtoto akamshika
Husaini akimtaka
Kijana kumuusiya
Huku mepiga pambaja
Na adui huko waja
Na huku akiwapiga
Mpaka mwisho kufikiya
Yakamzidi machungu
Akamsabihi Mungu
Akaaga Ulimwengu
Mjukuu wa Nabiya
Ghafula akijiliwa
Roho yake ikatwawa
Adui lake Moliwa
Imamu akamwendeya
Akamwendeya kwa dhati
Akamendesha mauti
Jiadui afiriti
Dharuba kumwemezeya
Alipokufa Husaini
Yalitimu thelathini
Na tatu yaliyo ndani
Mafumu yalowingiya
Kuna tena thelathini
Na nne mwake mwilini
Panga za hao wahuni
Mwilini zimesaliya
Mbali mengi majaraha
Kuyataja ni karaha
Moyo hauna furaha
Kwa Imamu kujifiya
Ndio huo mwisho wake
Hiki ndicho kisa chake
Cha Imamu tusichoke
Milele kujisomeya
Walipokwisha saini
Adui wakabaini
Sasa hii ni yakini
Ushindi umewajiya
Wakendewa majohari
Mabanati wa Amiri
Matekani wakaswiri
Huku wakiwachezeya
Pasi haya za uso
Wakaona ni kifani
Kuwatia taabani
Jamaa zake Nabiya
Wakazidisha jeuri
Wala pasipo na siri
Na kichwa chake Amiri
Fumoni wakakitiya
Huku wakikichezeya
Na huku wakiimbiya
Pasi imani kuwaingia
Wote wamefurahiya
Njiani walikipita
Nyoyo zao mezipata
Zimekwisha jaa vita
Shetwani amewaingiya
Alipopata habari
Kwa ambayo yamejiri
Yazidi akaamuri
Ili kwehwa kumwiliya
Furahani vibaraka
Haraka kukipeleka
Kwa Yazidi kikafika
Meyowe kufurahiya
Akawa akichezeya
Na vijiti kukitiya
Huku akimbiliya
Chini kukiumbiriya
Aso haya wala dini
Yazidi akatamani
Uchunguwe wa moyoni
Utatowa kwa duniya
Na huku akikigota
Meno akiyaambata
Uovu na usalata
Hakuna alodhaniya
Ajabu hii ajabu
Kwa kijanache swahibu
Kumfikiya ikabu
Wala pasipo hatiya
Muili ukiwa mbali
Kijana cha Murisali
Wakawachiwa mahuli
Na nyama kukitezeya
Basi haya ni mauti
Walotenda asherati
Lakini kwao laiti
Milele wamejutiya
Walitenda pasi haya
Dini kutotegemeya
Ya Mola kuyachezeya
Pasi nyuma kurejeya
Yapasa tuyalilie
Mauti yake Husaini
Islamu natulie
Kwa kifo chake Husaini
Hapa napenda kukoma
Hadithie kuisoma
Bali mengi sikusema
Dhiki nikiisikiya
Kisomoni waungwana
Majumbani na vijana
Mpate jua maana
Mambo yaliyotukiya
Yatupasa Isilamu
Machozi hadi ya damu
Kumliliya Imamu
Kwetu imetupasiya
Rabi atamtukuza
Peponi kum-bakiza
Kuzidi akimjaza
Neema kumshushiya
Hapa naweka kalamu
Nimefikiya makamu
Wala mbele siyo tamu
Hapa nitakomeleya