read

Aya 27 – 32: Watakaposimamishwa Motoni

Na ungeliona watakapoonyeshwa moto.

Mwenyezi Mungu (s.w.t) amerudia kuelezea hali ya wakadhibishaji Siku ya Kiyama, na kwamba wao watakapoona adhabu waliyoandaliwa na thawabu walizoandaliwa waumini, watasema:

Laiti tungerudishwa duniani wala hatutakadhibisha ishara za Mola wetu na tutakuwa katika wanaoamini.

Yaani tutatubia na tufanye amali njema. Lakini masikitiko na mazingatio hayafai chochote ila ikiwa kumwogopa Mwenyezi Mungu na adhabu yake ni kabla ya kutokea adhabu. Ama baada ya kutokea, basi ni kulilia maiti na kusikitika yaliyofutu.

Bali yamewadhihirikia waliyokuwa wakiyaficha zamani.

Hataokoka kesho na adhabu ya Mwenyezi Mungu ila ambaye yuko wazi katika maisha haya, vitendo vyake vinaambatana na kauli yake; yote mawili yawe ni picha ya dhati yake na hali yake, mpaka viwe vyote ni kama kitu kimoja tu mbele ya Mwenyezi Mungu na watu.

Ama yule mwenye kuzibaziba, ambaye Muumba anayajua yale ayafanyayo na watu hawayajui, miongoni mwa ria na unafiki, huyu yatamdhihirikia malipo ya ria yake na unafiki wake; na nafsi yake itajutia uovu wake na kutamani kujisafisha kwa kurudishwa duniani, lakini wapi!

Na kama wangalirudishwa, bila shaka wangeyarudia yale waliyokatazwa na hakika wao ni waongo.

Katika kusema kwao: Laiti tungerudishwa wala hatutakadhibisha ishara za Mola wetu na tutakuwa katika wanaoamini.

Tumesoma habari za wakosaji kadhaa ambao wanatubia wakiwa gerezani, lakini wanapotoka hurudia makosa yao. Mwenyezi Mungu anasema:

وَإِذَا مَسَّكُمُ الضُّرُّ فِي الْبَحْرِ ضَلَّ مَنْ تَدْعُونَ إِلَّا إِيَّاهُ ۖ فَلَمَّا نَجَّاكُمْ إِلَى الْبَرِّ أَعْرَضْتُمْ ۚ وَكَانَ الْإِنْسَانُ كَفُورًا {67}

“Na inapowafikia dhara katika bahari hupotea wale mnawaomba isipokuwa Yeye tu, lakini anapowaokoa mkafika salama nchi kavu mnageuka; na mwanadamu ni mkanushaji mno.” (17:67)

Na kusema: Hakuna kingine ila maisha yetu ya dunia, wala sisi hatutafufuliwa.

Yaani lau wangelirudishwa kwenye maisha yao ya mwanzo wangalisema waliyoyasema mwanzo: Hakuna ufufuo wala hisabu wala malipo.

Unaweza kuuliza: Vipi watakanusha na hali wao watakuwa wameshuhudia vituko vikubwa na wakaonyeshwa, mpaka wakataka kujitakasa nayo na kuahidi kuwa hawatarudia?

Jibu: Wao wanajua fika kwamba hisabu na adhabu itakuwa tu, hapana budi. Wakati huo huo wanajua kuwa lau wataitangaza haki na kuinyenyekea, chumo na faida zao watazikosa. Mwenyezi Mungu Mtukufu anasema:

وَجَحَدُوا بِهَا وَاسْتَيْقَنَتْهَا أَنْفُسُهُمْ ظُلْمًا وَعُلُوًّا ۚ{14}

“Na wakazikanusha (ishara zetu) na hali yakuwa nafsi zao zina yakini nazo kwa dhulma na kujivuna (27:14)

Na ungeliona watakaposimamishwa mbele ya Mola wao, baada ya kukadhibisha kukutana naye. Atasema: Je, si kweli haya?

Katika kufasiri Aya ya nne katika Sura hii tulisema kuwa Mwenyezi Mungu analingania kuamini haki pamoja na kusimamisha dalili yake. Mpingaji akiipinga, hoja inakuwa juu yake. Na Aya hii inatilia mkazo hilo na kutaja dalili na hoja walizozikanusha na kuzikadhibisha.

Watasema: Kwanini? Tunaapa kwa Mola wetu.

Hivi sasa yamepita yaliyopita na hakuna kilichobaki isipokuwa malipo yenye kulingana na adhabu kwa mwenye kukufuru na kukanusha.

Akasema: Basi onjeni adhabu kwa sababu ya mliyokuwa mkikataa.

Hayanimalipoyakilamwenyekuiwekambeledunianakuiacha Akhera na akaificha haki kwa hawa ya nafsi yake.

Utauliza: Kauli yake Mwenyezi Mungu kwa Makafiri: ‘Je, si kweli haya?’ Na kauli yake: “Onjeni adhabu” mbona haziafikiani na kauli yake:

وَلَا يُكَلِّمُهُمُ اللَّهُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ{174}

Wala hatawasemeza Mwenyezi Mungu Siku ya Kiyama.”? (2:174)

Jibu: Makusudio ni kwamba Mwenyezi Mungu hatawasemesha yale yanayowafurahisha, bali atawasemeza yanayowaudhi, kama ilivyo katika Aya hii, na ilivyo katika Aya isemayo:

قَالَ اخْسَئُوا فِيهَا وَلَا تُكَلِّمُونِ {108}

“Atasema: Tokomeeni humo wala msinisemeze.”(23:108)

Hakika wamekwishahasirika wale waliokadhibisha kukutana na Mwenyezi Mungu na wamefuzu wale waliomwamini, mpaka itakapowajia ghafla saa (Kiyama) watasema: Oo! Majuto yetu juu ya yale tuliyoyapuza!

Imam Ali anasema: “Matunda ya kupuuza ni majuto, na matunda ya uthabiti ni amani.”

Nao watabeba mizigo yao migongoni mwao. Angalieni! Ni mabaya mno wanayoyabeba.

Mizigo ni dhambi na kuibeba mgongoni ni fumbo, yaani kuwa nayo; kama vile isemwavyo: “Amepandwa na shetani.” Yaani yuko naye hamwachi. Maana ni kuwa wanaoikadhibisha haki ndio watu wenye hali mbaya zadi huko akhera.

Mmoja wa wafasiri wapya anasema: “Bali mnyama ana hali nzuri zaidi kwa sababu hubeba mizigo mizito,; na mnyama huutua mzigo wake akaenda kupumzika, lakini hawa watakwenda na mizigo yao kwenye Jahannam wakisindikizwa na dhambi.”

Na maisha ya dunia si kitu ila mchezo na upuzi.”

Umetangulia mfano wake katika Juz 4 (3:185)

قَدْ نَعْلَمُ إِنَّهُ لَيَحْزُنُكَ الَّذِي يَقُولُونَ ۖ فَإِنَّهُمْ لَا يُكَذِّبُونَكَ وَلَٰكِنَّ الظَّالِمِينَ بِآيَاتِ اللَّهِ يَجْحَدُونَ {33}

Hakika tunajua kwamba yanakuhuzunisha yale wanayoyasema. Basi hakika hao hawakukadhibishi wewe, lakini madhalimu wanakataa ishara za Mwenyezi Mungu.

وَلَقَدْ كُذِّبَتْ رُسُلٌ مِنْ قَبْلِكَ فَصَبَرُوا عَلَىٰ مَا كُذِّبُوا وَأُوذُوا حَتَّىٰ أَتَاهُمْ نَصْرُنَا ۚ وَلَا مُبَدِّلَ لِكَلِمَاتِ اللَّهِ ۚ وَلَقَدْ جَاءَكَ مِنْ نَبَإِ الْمُرْسَلِينَ {34}

Na hakika walikadhibishwa Mitume kabla yako, wakavumilia juu ya kukadhibishwa na kuudhiwa, mpaka ikawafikia nusura yetu. Na hakuna wa kubadilisha maneno ya Mwenyezi Mungu. Na bila shaka zimekujia baadhi ya habari za Mitume hao.

وَإِنْ كَانَ كَبُرَ عَلَيْكَ إِعْرَاضُهُمْ فَإِنِ اسْتَطَعْتَ أَنْ تَبْتَغِيَ نَفَقًا فِي الْأَرْضِ أَوْ سُلَّمًا فِي السَّمَاءِ فَتَأْتِيَهُمْ بِآيَةٍ ۚ وَلَوْ شَاءَ اللَّهُ لَجَمَعَهُمْ عَلَى الْهُدَىٰ ۚ فَلَا تَكُونَنَّ مِنَ الْجَاهِلِينَ {35}

Na ikiwa ni makubwa kwako huku kukataa kwao, basi kama unaweza kutafuta njia ya chini kwa chini katika ardhi au ngazi kwendea mbinguni na kuwaletea ishara. Na kama Mwenyezi Mungu angelitaka, bila shaka angeliwakusanya kwenye uongofu. Basi usiwe miongoni mwa wajinga

إِنَّمَا يَسْتَجِيبُ الَّذِينَ يَسْمَعُونَ ۘ وَالْمَوْتَىٰ يَبْعَثُهُمُ اللَّهُ ثُمَّ إِلَيْهِ يُرْجَعُونَ {36}

Hakika wanaokubali ni wale tu wanaosikia. Na wafu Mwenyezi Mungu atawafufua kisha watarejeshwa kwake.

وَقَالُوا لَوْلَا نُزِّلَ عَلَيْهِ آيَةٌ مِنْ رَبِّهِ ۚ قُلْ إِنَّ اللَّهَ قَادِرٌ عَلَىٰ أَنْ يُنَزِّلَ آيَةً وَلَٰكِنَّ أَكْثَرَهُمْ لَا يَعْلَمُونَ {37}

Na husema: Kwa nini hakuteremshiwa ishara kutoka kwa Mola wake? Sema: Hakika Mwenyezi Mungu ni mwenye uweza wa kuteremsha ishara yoyote, lakini wengi wao hawajui.