read

Aya 87 – 88:Tulimpa Musa Kitabu

Lugha

Neno Maryam, lina maana ya mtumishi kwa lugha ya kiebrania. Kwa sababu mama yake Maryam aliweka nadhiri ya kumtoa awe mtumishi wa Baitul-Maqdis (Quds).

Na hakika tulimpa Musa Kitabu na tukawafuatisha Mitume baada yake

Yaani tumempa Musa Tawrat; kisha tukawapeleka Mitume baada yake, mmoja baada ya mwengine. Inasemekana kuwa hazikupita zama kati ya Musa na Isa ambaye ndiye Mtume wa mwisho wa Kiisrail, isipokuwa kulikuwa na Mtume Mursal au Mitume tofauti wanaoamrisha mema na kukataza mabaya. Imesemwa katika Tafsirul Razi na ya Abu Hayan El-Andalusi kwamba Mitume hao ni Yoshua, Samuel, Sham’un, Daud, Suleiman, na Shiau. Vile vile Armiya, Uzayr, Ezekiel, Eliyas, Yunus, Zakaria na Yahya.
Na tukampa Isa mwana wa Maryam, hoja zilizo wazi wazi na tukamatia nguvu kwa ro ho takatifu.

Isa (a.s.) ndiye Mtume wa mwisho wa wana wa Israil, na kati yake na Musa kulikuwa na karne 14.

Ni kidogo tu wanayoamini

Yaani hawakuamini katika Mayahudi isipokuwa wachache tu, kama Abdallah bin Salam na wafuasi wake. Mwenye Majmaul-Bayan amechagua kusema kuwa maana ya: “ni kidogo tu wanayoamini” kwamba hakuamini yoyote katika wao, si wachache wala wengi; kama vile inavyosemwa ni nadra kufanya’. Kwa maana ya kutofanya kabisa. Lakini maana tuliyoyaeleza mwanzo ndiyo yaliyo sahihi zaidi, kwa kuangalia kauli yake Mwenyezi Mungu:

وَقَوْلِهِمْ قُلُوبُنَا غُلْفٌ ۚ بَلْ طَبَعَ اللَّهُ عَلَيْهَا بِكُفْرِهِمْ فَلَا يُؤْمِنُونَ إِلَّا قَلِيلًا {155}

...Na kwa kusema kwao nyoyo zetu zimefumbwa, bali Mwenyezi Mungu amezipiga mhuri kwa kufuru yao, basi hawataamini ila wachache tu.” (4:155).

Mkweli Na Tapeli

Inatakikana tuangalie tena kuhusu kauli ya Mwenyezi Mungu: “Kila walipowafikia Mitume ...” mpaka mwisho. Hakika Aya hii tukufu pamoja na kuwa na madhumuni ya kumsuta mwenye kuwaasi Mitume na kuikataa haki, kama haikuafikiana na matakwa yake, pia vile vile ina madhumuni ya kumsuta mwenye kuwapuuza watu na asiwakabili kwa tamko la haki kwa kutaka kujipendekeza kwao kwa tamaa ya cheo nk.

Hakika mtengenezaji wa kweli anaizungumza haki wala haogopi lawama katika kazi ya Mwenyezi Mungu. Kwa sababu lengo lake la kwanza na la mwisho ni kumridhisha Mwenyezi Mungu peke yake. Kwa ajili hiyo ndio anajitoa muhanga na kufa shahidi kwa ajili ya kuwapelekea na kuwaonyesha haki umma. Ama mharibifu aliye mwongo anakuwa na lengo la kuwaridhisha watu ili wanunue bidhaa yake: Imam Ali (a.s.) anasema: “Usimchukize Mwenyezi Mungu kwa kumridhisha yeyote katika viumbe vyake.”

وَلَمَّا جَاءَهُمْ كِتَابٌ مِنْ عِنْدِ اللَّهِ مُصَدِّقٌ لِمَا مَعَهُمْ وَكَانُوا مِنْ قَبْلُ يَسْتَفْتِحُونَ عَلَى الَّذِينَ كَفَرُوا فَلَمَّا جَاءَهُمْ مَا عَرَفُوا كَفَرُوا بِهِ ۚ فَلَعْنَةُ اللَّهِ عَلَى الْكَافِرِينَ {89}

Na kilipowajia kitabu kitokacho kwa Mwenyezi Mungu kisadikishacho yaliyo pamoja nao, na zamani walikuwa wakiomba ushindi juu ya mkafiri. Lakini yalipowafikia yale waliyoyajua waliyakataa. Basi laana ya Mwenyezi Mungu iko juu ya makafiri.

بِئْسَمَا اشْتَرَوْا بِهِ أَنْفُسَهُمْ أَنْ يَكْفُرُوا بِمَا أَنْزَلَ اللَّهُ بَغْيًا أَنْ يُنَزِّلَ اللَّهُ مِنْ فَضْلِهِ عَلَىٰ مَنْ يَشَاءُ مِنْ عِبَادِهِ ۖ فَبَاءُوا بِغَضَبٍ عَلَىٰ غَضَبٍ ۚ وَلِلْكَافِرِينَ عَذَابٌ مُهِينٌ {90}

Kibaya kabisa walichokiuzia nafsi zao ni kule kukataa kile alichokiteremsha Mwenyezi Mungu kwa kuona maya kuwa Mwenyezi Mungu amemteremshia fadhila zake amtakaye katika waja wake. Kwa hiyo wakastahili ghadhabu juu ya ghadhabu, na watakuwa nayo makafiri adhabu idhalilishayo.

وَإِذَا قِيلَ لَهُمْ آمِنُوا بِمَا أَنْزَلَ اللَّهُ قَالُوا نُؤْمِنُ بِمَا أُنْزِلَ عَلَيْنَا وَيَكْفُرُونَ بِمَا وَرَاءَهُ وَهُوَ الْحَقُّ مُصَدِّقًا لِمَا مَعَهُمْ ۗ قُلْ فَلِمَ تَقْتُلُونَ أَنْبِيَاءَ اللَّهِ مِنْ قَبْلُ إِنْ كُنْتُمْ مُؤْمِنِينَ {91}

Na wakiambiwa: Yaaminini aliyoyateremsha Mwenyezi Mungu husema: Tunaamini yaliyoteremshwa juu yetu; na hukataa yaliyo nyuma yake; na hali yakuwa hii ndiyo haki inayosadikisha yaliyo pamoja nao. Sema: Mbona mliwaua Mitume wa Mwenyezi Mungu hapo zamani kama mlikuwa mkiamini